24 May, 2024

Elementor #142

PACSO KUPITIA MRADI WA URAIYA WETU WANAWAPATIA MAFUNZO AFSA USTAWI WA JAMII

17 Nov, 2023

PACSO: ‘TUNATEKELEZA KWA VITENDO MAONO YA DK. MWINYI, DK. SAMIA’

MRATIBU wa miradi kutoka Mwenvuli wa asasi za kiraia Pemba ‘PACSO’ Mohamed Najim Omar, alisema wanatekeleza kwa vitendo, maono ya Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan, la kuhakikisha elimu ya uraia na demomkrasia inawafikia wananchi.

Mratibu huyo aliyasema hayo, wakati akizungumza na watendaji wa serikali na wanaasasi za kiraia, katika kongamano la pamoja, la kujenga ushirikiano, baina pande mbili hizo, kupitia mradi wa ‘uraia wetu’ lililofanyika Wawi Chake chake.

Alisema, mradi huo ni tokeo moja wapo la maono ya viongozi hao, ambapo wameamua kuwakusanya watendaji wa serikali na wale wa asasi za kiraia, ili kuibua changamoto zinazokwamisha ushirikiano wao.

Alieleza kuwa, washiriki wa kongamanio hilo, watapata nafasi ya kuelezea changamoto zao kikanuni, sera na kisheria ili kuona zinatatuliwaje kwa umoja wao.

‘’Sote ni mashahidi kuwa, wakati viongozi wetu wanaingia madarakani, walihimiza mno suala la kuzifahamu sheria, kuona changamoto zake na hata kuzifanyia marekebisho, ili kusiwe na mkwamo katika utekelezaji wa shughuli husika,’’alieleza.

Aidha Mratibu huyo wa miradi kutoka ‘PACSO’ Mohamed Najim Omar, alieleza kuwa washiriki watachambua sera, kanuni na sheria ambazo wakati wanapotekeleza majukumu yao, zinawakwaza.

 

 

Katika hatua nyingine alifafanua kuwa, PACSO imeandaa jukwaa la kuwakutanisha pamoja watendaji wa serikali na wanaasasi za kiraia, ili kujadili kwa pamoja changamoto za watu wenye ulemavu, vijana na wanawake.

Alieleza kuwa, maoni ambayo yatapatikana katika kongamano hilo, watayaandika vyema na kuyasilisha kwa Jumuiya ya wanawake wanawake wenye ulemavu Zanzibar, ambao nao watakeleza mradi kama huo, ngazi ya kitaifa.

‘’Kwenye mradi huu PASCO, inatekeleza ngazi ya kanda (zone), ingawa wenzetu wa JUWAUZA wanatekeleza ngazi ya kitaifa na kisha maoni hayo, watayafikisha kwa viongozi wa kitaifa,’’alieleza.

Akifungua kongamanio hilo, Msaidizi Naibu Mrajisi wa Asasi za Kiraia Pemba, Saada Abubakar Khamis, alisema mradi huo, unaweza kuleta tija, kwa vile unaangalia kwa upana wake, suala la demokrasia.

Alieleza kuwa, moja ya chanagamoto iliyopo ni kutoonekana kwa uhusiano mzuri, baina ya asasi za kiraia na serikali kuu, jambo ambalo wakati mwengine huchelewa kutekelezwa kwa miradi.

‘’Jambo hili lililofanywa na wenzetu ‘PACSO’ naamini litazidisha ushirikiano na uhusiano mzuri uliopo baina ya serikali na asasi za kiraia, hasa kwa vile pia litaangalia sheria na kanuni zinazokwamisha utendaji wa asasi,’’alifafanua.

Alifafanua kuwa, demokrasia ni dhana pana na wakati mwengine wapo wanaoona inahusu ngazi za juu pekee, bila ya kuona kuwa dhana hiyo, hutakiwa kuonekana hata kwenye asasi za kiraia.

Wakichangia kwenye kongamano hilo, washiriki hao walisema ushirikishwaji ni jambo jema, katika kufikia uamuzi wowote, katika nchi ama asasi za kiraia.

Afisa wa watu wenye ulemavu wilaya ya Chake chake Mwadini Ali Juma, alisema bado watu wenye ulemavu, hawajatendewa haki sana katika ajira, miundombinu na majengo ya umma.

Mwakilishi kutoka TAMWA, Asha Mussa Omar, alisema kikwazo kilichopo ni kwa jamii, kutotaka kubadili mitazamo, juu ya dhana ya mwanamke na uongozi.

‘’Wapo baadhi ya watu wanawavunja moyo wanawake, kwa kuwaambia kuwa wakiwa viongozi, watakuwa wamevunja maadili, watapewa takala, dhana hizi zinahitaji elimu kwa bidii,’’alieleza.

Akiwasilisha mada ya umuhimuwa ushirikiano baina ya asasi za kiraia na serikali, mkufunzi Juma Bakar Alawi, alisema hakuna haja ya pande mbili hizo, kunyimana taarifa.

Alieleza kuwa, asasia zote za kiraia Zanzibar, zinatekeleza miradi ambayo ni maono ya serikali kuu, hivyo ni vyema pande moja wapo inapohitaji taarifa, iwe rahisi kupeana.

Kongamano hilo la siku moja, kupitia mradi wa ‘uraia wangu’ limeandaliwa na kufadhiliwa na The Foundation for Civil Society kupitia Umoja wa nchi za Ulaya.

10 Oct, 2023

JAMII YAKUMBUSHWA KUILINDA HAKI KUU YA BINAADAMU

JAMII imekumbushwa kuwa, moja ya haki kuu ya msingi kwa kila mwanadamu ni ile ya kuishi, hivyo ni kosa kwa mtu mwengine yeyote kumuondolea mwenzake.

Hayo yalielezwa na mtoa mada mwanasheria kutoka Shirika la Msaada na Haki za Binaadamu Siti Habib Mohamed, wakati akiendesha mafunzo ya siku nne kwa waandishi wa habari, wadau wa habari na wasaidizi wa sheria, yanayofanyika Chuo cha Amali Vitongoji Chake chake na kuandaliwa na Mwemvuli wa asasi za Kirai Pemba PACSO kwa ufadhili wa UNDP.

Alisema kua zana ya haki za binadamu ilianzishwa mnamo  mwaka 1948 baada ya vita vya kwanza vya dunia, hivyo ni wajibu wa kila mmoja hadi leo hii, kuhakikisha anailinda na kuitetea haki ya kuishi ya mwanzake.

Alieleza kuwa, haki za binadamu kimsingi ni yale madai au haki zote ambazo anadai binamu mara baada ya kuzaliwa, na kwa kawida hakuna taasisi yoyote ambayo inaweza kuzuia.

‘’Ni kweli haki ya msingi kwa kila mwanadamu ni ile ya kuishi, hivyo ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha anailinda yake mwenyewe na mwenzake,’’anaelkeza.

Hata hivyo alieleza kua kupitia Mkataba wahaki za  binadamu ambao uliasisiwa mwaka 1966 na kuanza kufanyaka kazi mwaka 1976, umeanisha haki nyingine kadhaa za binadamu kama vile kutoa maoni.

Katika hatua nyingine mtoa mada huyo alieleza kua zipo hatua mbali mbali, ambazo zimekuja kwa ajili ya kuzilinda haki hizo ikiwa ni pamoja na kuanzishwa wizara maalum, kuanzishwa kwa tume ya Haki za binadamu na utawala bora.

‘’Lakini hata kuingizwa kwenye katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na ile ya Zanzibar ya mwaka 1894 na uwepo wa wizara husika na asasi ni sehemu ya kuzilinda,’’alifafanua.

Mapema Mkurugenzi wa PACSO Mohamed Najim Omar, alisema waliona wakutane na waandishi wa habari, wanaharakati wa haki za binadamu na wasaidizi wa sheria, ili kuwajengea uwezo.

‘’Waandishi wananafasi kubwa ya kuhakikisha wanakemea matendo ya uvunjifu wa haki za binadamu kupitia kazi zao,’’alieleza.

Washiriki wa mafunzo hayo walisema bado elimu inahitajika kwa jamii, ili wafahamu athari za uvunjifu wa haki za binadamu.

Mshiriki kutoka chama cha ACT Wazalendo Saleh Nassor Juma, waliishukuru taasisi hii ya PACSO kwa kuwapa mafunzo hayo, ambayo yamewapa uwelewa zaidi.

Nae mtaangazaji wa Redio Istiqama Pemba Bakar Khamis Juma, alisema kama mataifa makubwa, yatajenga utamaduni wa kuziheshimu haki za binadamu dunia itakuwa salama.

Nao washiriki Abubakar Mohamed Ali ,Mwache Juma Abdalla walisema, kama vyombo vya habari vitakuwa huru kufanya kazi, wanaweza kukemea matendo ya uvunjifu wa haki za binadamu yanayojitokeza.

Mratibu wa miradi kutoka Shirika la Maendeleo Ulimwenguni la UNDP Gamalick Sun  alisema wataendelea kuiunga mkono PACSO katika shughuli zao mbali mbali.

Alieleza kuwa, anaamini PACSO ni sehemu ya uwakilishi wa wananchi, na ndio maana hata mafunzo hayo yamewashirikisha watu wa kada mbali mbali.

Mafunzo hayo ya siku nne mada kadhaa zitajadiliwa ikiwa ni pamoja na uhuru wa kujieleza, haki za binaadamu, majukumu ya waandishi wa habari na jukumu la jamii katika kulinda haki za binaadamu,.

10 Aug, 2023

PACSO YAWAONESHA NJIA YA MALEZI WAZAZI, WALEZI PEMBA

JAMII kisiwani Pemba, imetakiwa kufahamu changamoto na viashiria vya udhalilishaji kwa watoto, ili kuwalinda na vitendo hivyo.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Mtandao wa Asasi za Kiraia Pemba ‘PACSO’ Mohamed Ali Khamis, mara baada ya kuutambulisha mradi wa kujadili changamoto zinazowakabili watoto, katika ukumbi wa kiwanda cha Makonyo Wawi Chake chake Pemba.

Alisema, jamii inapaswa kuwa karibu mno na watoto wao, ili kujua haraka viashiria vya kudhalilishwa, na sio kusubiri hadi janga liwakumbe.

Mwenyekiti huyo alieleza kuwa, hilo litakuwa rahisi ikiwa wazazi na walezi watatenga muda wa kuwa karibu na watoto wao.

‘’Kama tunajiona tuko na harakati nyingi za maisha na kusahau kukaa na watoto wetu, wanaweza kukumbwa na janga kama la udhalilishaji na tukachelewa kufahamu,’’alieleza.

Akielezea lengo la mradi huo Mwenyekiti huyo wa PACSO, alisema ni kuwazindua wazazi, kufahamu viashiria na changamoto na namna ya kuwasaidia watoto wasifanyiwe matendo hayo.

Akifungua mafunzo hayo, Mratibu katika ofisi ya usajili wa asasi za kiraia Pemba, Ashrak Hamad Ali, alisema baadhi ya wazazi wanakosa muda wa kukaa na watoto wao, ili kusikiliza changamoto zinazowakabili.

Aidha aliwataka wazazi kujenga utamaduni wa kukaa na watoto wao ili kuwapa fursa ya kuwasikiliza sambamba na kufuatilia nyenendo zao za kila siku.

Katika hatua nyingine, Mratibu huyo, aliwataka waandishi wa habari kushirikiana na viongozi wa dini, kutoa elimu kwa wanandoa, ili kupunguza talaka za kiholela.

‘’Wakati mwengine wapo watoto wetu wanakumbana na changamoto za kimaisha na kisha kudhalilishwa ama kutelekezwa, moja ya sababu ikiwa ni wazazi kutengana,’’alifafanua.

Akiwasilisha mada kwenye mkutano huo kuhusu changamoto zinazowakabili watoto, Mratibu kutoka Chama cha waandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA– Pemba Fat- hyia Mussa Said, alisema watoto wana haki ya kushiriki na kushirikishwa kwenye ngazi za kijamii.

Akizitaja baadhi ya haki hizo kupitia mkataba wa kimatifa wa mwaka 1988 ni pamoja na ya kuishi, kuendelezwa kwa mujibu wa sera ya maendeleo ya mtoto Tanzania, kulindwa na vitendo viovu pamoja na haki ya kushirikishwa.

Nao washiriki wa mkutano huo, Aisha Abdallah Juma na mwenzake Abdurr-azak Imam Juma, walisema ni hatari kwa wazazi kupuuzi taarifa wanazopewa na watoto wao.

Sheha wa shehia ya Pembeni wilaya ya Wete Saumu Ali Hamad na mjumbe wa sheha shehia ya Wambaa Amini Haji Makame, walisema kukosekana kwa uthubutu wa wazazi, kuwakemea watoto kuiga mitindo ya kigeni ni moja ya chanzo cha kutokea kwa changamoto hizo.

Awali, Mratibu wa miradi kutoka PACSO Mohamed Najim Omar, alisema kama jamii haikuungana kama ilivyokuwa zamani kwenye malezi, watoto wataendelea kukumbwa na changamoto.

Aidha aliwataka washiriki wa mkutano huo, kuisambaaza elimu walioipata, ili kuona wazazi na walezi wanakuwa na mamko wa malezi kwa watoto wao.

Mradi huo wa miezi sita unatekelezwa kwa ufadhili wa Shirika la Irish Aid, unaendeshwa na Mtandao wa Asasi za Kiraia Pemba ‘PACSO’.

10 Feb, 2022

IRELAND YARIDHISHWA UTEKELEZAJI MRADI WA ARDHI PACSO

NAIBU Balozi wa Ireland nchini Tanzania Mags Gaynor, ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa umiliki wa rasilimali ardhi kwa wanawake, uliokuwa ukitekelezwa na Mwemvuli wa asasi za kirais Pemba ‘PACSO’ na kumalizika hivi karibuni.

Naibu Balozi huyo alisema, kutokana na majibu ya wanufaika wa mradi huo alivyozungumza nao, ameridhishwa na utekelezaji wa mradi huo, na hasa kwa kuwafikia walengwa.

Alisema mradi huo ulilenga kuwafikia wanawake ili kuwajengea uwelewa, juu ya umilikiwa wa rasilimali ikiwemo ardhi, jambo ambalo sasa, limewanufaisha hasa kwa kuwepo wanufaika waliopata haki zao.

Naibu Balozi huyo aliyasema hayo ofisi za PACSO Chake chake Pemba, kwenye kikao cha tathimi kilichojumuisha wanufaika wa mradi wa uongozi wa PACSO.

Alieleza kuwa, kwa vile wapo wanawake kisiwani Pemba walionufaika moja kwa moja, ikiwa ni pamoja na kurithi, kununua ardhi na kulalamikia ucheleweshaji urithi ni hatua kubwa.

“Serikali ya Ireland, imeridhishwa mno na mradi huu uliokuwa ukiendeshwa na ‘PACSO’ na tutangalia uwezekano wa kuendeleza kuhusiasna na elimu kwa jamii,’’alieleza.

Katika hatua nyingine, Naibu huyo Balozi wa Ireland Mags Gaynor, alisisitiza haja kwa wanufaika hao kuwafikishia wenzao elimu ya umuhimu wa umiliki rasilimali.

Alisema kuwapa mradi huo PACSO rasilimali fedha hazikupotea, kutokana na kuwanufaisha walengwa, waliokuwasudiwa ndani ya jamii husika.

Mmoja wa wanufaika hao Fatma Khamis Juma wa Wawi, alisema awali hakuwa akiona umuhimu wa umiliki wa rasilimali, ingawa baada ya mafunzo, sasa ameamka.

“Hata urithi sasa tumesharithi, maana niliwaambia kaka zangu kuwa sasa turithi, na tumesharithi baada ya kuwaelimisha ingawa walikuwa wazito,’’alieleza.

Mratibu wa miradi kutoka PACSO, Mohamed Najim Omar, alisema licha ya mradi huo kuwa wa miezi miwili, lakini umefikia lengo lao.

“Pamoja na kwamba mradi ulikuwa wa miezi mwili, lakini wanawake kwa asilimia 60 na wanaume asilimia 40, walifikiwa na kunufaika kwa kupata elimu,’’alieleza.

Nae Salama Mtondoo kutoka Wete, alisema licha ya kuwa na kesi yake mahakamani ya kutapeliwa na kiongozi wa serikali ardhi yake, lakini mafunzo hayo yamempa hamasa zaidi.

“Mafunzo ya umiliki wa ardhi, na hasa siku ile ya kuzitambua sheria za ardhi, kwangu yamenipa uwelewa zaidi, wa kuendelea na kesi yangu,’’alieleza.

Sheha wa shehia Vitongoji wilaya ya Chake chake, Ayoub Suleiman, alisema katika kipindi cha mwezi Januari hadi Febuari alipokea malalamiko 40 ya wanawake juu ya ardhi.

“Baada ya kupata mafunzo ya umiliki wa rasilimali hasa ardhi, sasa hata malalamiko katika shehia yangu yameongezeka kutoka 25 ya mwaka 2021, hadi kufikia 40 kwa kipindi cha miezi mwili kwa mwaka huu,”alisema.

 

Afisa Mipango wilaya ya Chake chake Kassim Ali Omar, alisema wamepokea maombi 20 kwa mwaka huu, ya wanawake wakiomba kununua na kuuza ardhi zao.

Katibu mkuu wa ‘PACSO’ Sifuni Ali Haji, alisema mradi huo wanatarajia unawezaa mwengine kutokana na mafanikio makubwa waliyoyapata.

Katika utekelezaji wa mradi huo, awali kulifanyika uzinduzi wa mradi, kongamano, mafunzo ya siku nne ya umiliki ardhi pamoja na kuzifahamu sheria za usimamizi ardhi.